Wanasiasa Marekani waomboleza kifo cha Seneta John McCain
Wanasiasa nchini Marekani wakiongozwa na rais Donald Trump wamekuwa wakimimina salamu za rambirambi kwa familia ya Seneta wa Chama cha Republican na mkosoaji mkubwa wa Utawala wa Rais Donald Trump, John McCain aliyeaga dunia mapema hii leo.
Imechapishwa:
McCain, mfungwa wa kivita wakati wa vita ya Vietnam ameaga dunia asubuhi ya leo kwa saa za Marekani akiwa na umri wa miaka 81 baada ya kusumbuliwa na kansa ya ubongo kwa zaidi ya mwaka mmoja, taarifa ya ofisi yake imeeleza.
Taarifa ya kifo chake imefafanua kwamba kiongozi huyo aliaga dunia akiwa amezungukwa na familia yake akiwemo mkewe, Cindy.
Rais wa Marekani, Donald Trump ametoa salamu za pole kwa faimilia ya McCain, akieleza wamarekani wote wako pamoja kufuatia msiba huo.
Aidha, Marais wastaafu wa Marekani Bill Clinton na Barrack Obama pia wametuma salamu za rambirambi wakimuelezea McCain kuwa kiongozi wa mfano aliyekuwa mstari wa mbele kuipigania na kuitetea nchi ya marekani.
Kisiasa McCain atakumbukwa alipowania urais wa Marekani mwaka 2008 na kushindwa na Obama, aidha amehudumu kama gavana wa Arizona kwa zaidi ya miongo mitatu.
Hata hivyo wakosoaji walimshutumu kwa kuwa mstari wa mbele kutetea ujenzi wa makazi ya katika Ukanda wa Gaza na pia kuunga mkono azimio la Marekani la kuutambua mji wa jerusalem kama Mji Mkuu wa Israel.