Anthony Joshua aomba Pambano dhidi ya Fury
NAIROBI – Baada ya muda mrefu Anthony Joshua maarufu kama ‘AJ’ amerudi katika kiwango chake cha ubabe baada ya kushinda pambano lake dhidi ya Jermaine Franklin wikiendi iliyopita.
Imechapishwa:
Pambano hili liliandaliwa katika ukumbi wa 02 Arena mjini London, ambapo Anthony alishinda kwa kura za majaji wote watatu (UD).
Ushindi huo sasa umempa nguvu mpya AJ na kutangaza hadharani anamhitaji Mwingereza mwenzake, Tyson Fury kupimana nguvu.
Kwa mujibu wa AJ anamhitaji Fury ili wapambane ulingoni kukata kiu ya mashabiki wao waliowakosa mwaka 2021 kama ilivyowahi kukubaliwa baina yao.
Safari hii kama pambano litapangwa, wataushindania mkanda wa WBC alionao Fury. Hii itakua tofauti na ilivyokuwa wakati ule AJ alipokuwa na mikanda mitatu ya uzito wa juu.
Kufikia sasa bado Pambano la Fury na Oleksandr Usyk halijathibitika kuwepo baada ya Kuvunjika kwa makubaliano ya pambano hilo.
Promota wa Usyk, Alex Krassyuk kwa sasa anafikiria uwezekano wa kujadili mpango wa pambano dhidi ya Daniel Dubois ili mteja wake atetee mkanda wake wa WBA.