Nigeria kuandaa fainali ya kombe la Shirikisho barani Afrika
Na: Paul Nzioki
Imechapishwa:
Fainali ya Kombe la Shirikisho baina ya vlabu itachezwa Mei 20, 2022 kwenye Uwanja wa Godswill Akpabio nchini Nigeria.
Hatua hii inakuja baada ya uamuzi huo kuchukuliwa na Shirikisho la soka barani Afrika CAF.
Hii ni fainali ya kwanza ya kimataifa kuchezwa katika uwanja wa nyumbani wa Akwa United, inayoshiriki ligi kuu nchini Nigeria.
Uwanja wa Kimataifa wa Godswill Akpabio, upo Uyo mji mkuu wa Jimbo la Akwa Ibom.
Kuelekea fainali
Katika mchezo wa ufunguzi wa mkondo wa kwanza wa nusu fainali, TP Mazembe ya DRC, ilipata ushindi wa bao 1-0 dhidi ya RS Berkane ya Morocco , goli la dakika za majeruhi kutoka kwa John Bakata.
Katika nusu fainali ya pili, mkondo wa kwanza kati ya Al Ahli Tripoli ya Libya na Orlando Pirates ya Afrika Kusini, vijana wa orlando wanaofunzwa na Mandla Ncikazi wana faida ya 2-0 ugenini katika mkondo wa pili.
Mechi za mkondo wa pili wa nusu fainali zitachezwa Jumapili Mei 15, 2022.
Raja Athletic ya Morocco iliibuka mabingwa mwaka jana (2021) baada ya kuifunga klabu ya Js kabylie ya Algeria mabao 2-1 kwenye fainali iliyochezwa Cotonou, Benin.