Hofu ya virusi vya Zika, yamfanya Rory McIlroy kujitoa
Wakati dunia ikijiandaa kukutana kama kijiji wakati wa michezo ya Olympic mjini Rio, Brazil, mchezaji gofu, Rory Mcllroy, ametangaza kujitoa kushiriki michezo ya mwaka huu kutokana na hofu ya virusi vya ugonjwa wa Zika.
Imechapishwa:
Kwenye taarifa yake aliyoitoa kwa vyombo vya habari, Mcllroy amesema kuwa "afya yangu na ya familiya yangu zinakuja kwanza kabla ya mambo mengine yote." alisema mchezaji huyo.
"Licha ya kuwa maambukizi ya virusi vya ugonjwa wa Zika yanaelezwa kuwa ni ya kiwango cha chini, bado ni hatari na ni hatari ambayo binafsi siko tayari kuichukua." alisema Mcllroy kwenye taarifa yake.
Wachezaji wengine kama Vijay Singh na Muastralia Marc Leishman wao walishatangaza toka awali kujiondoa kushiriki michezo ya mwaka huu ya Olympic, kwa hofu ya virusi vya Zika.
Mapema mwezi huu, bingwa huyo mara nne wa taji la dunia la mchezo wa gofu, Mcllroy, ambaye alikuwa aiwakilishe nchi ya Ireland kwenye michezo hiyo, alisema hofu kuhusu Zika ilikuwa imempungua.
Ugonjwa wa virusi vya Zika umekuwa ukihusishwa na madhara yanayotokana na wajawazito wakati wanapojifungua, watoto kuwa na vichwa vidogo.
Hata hivyo kamati ya maandalizi ua michezo ya mwaka huu mjini Rio, pamoja na shirika la afya duniani WHO, walisema kuwa wamehakikisha kuwa mbu wanaoambukiza ugonjwa huo wamedhibitiwa na hakuna hatarik yoyote.
Hata hivyo, hivi karibuni jopo la wataalamu huru wa afya dunia walikutana na kueleza hatari kubwa iliyopo ikiwa michezo hiyo itafanyika na kupendekeza iahirishwe na kupewa nchi nyingine kuiandaa.