Alonso: Nitashiriki mbio za Texas, Marekani licha ya majeraha ya mgongo
Dereva wa mbio za magari yaendayo kasi zaidi duniani ya Langalanga ama Formula One, Fernando Alonso amethibitisha kuwa atashiriki mbio za US Grand Prix zinazotarajiwa kufanyika mwishoni mwa juma hili licha majeraha ya mgongo.
Imechapishwa:
Alonso amesema kuwa atashiriki mbio hizo zilizopangwa kufanyika kwenye mji wa Austin jimboni Texas mwishoni mwa juma baada ya kupata nafuu ya kutosha kutokana na ajali aliyoipta juma moja lililopita.
Dereva huyo aliumia mgongo kwenye mashindano ya Abu Dhabi yaliyofanyika juma moja lililopita baada ya gari lake kugongana na gari jingine likiwa kwenye mwendo wa maili 150 kwa saa.
Fernando alilazimika kukimbizwa hospitalini baada ya ajali hiyo lakini baadae aliruhusiwa kutoka hospitali baada ya kubainika kuwa hakuumia sana sehemu ya mgongo wake.
Kulikuwa na hatihati ya mkimbiza magari huyu kutoshiriki mbio za Marekani kutokana na jeraha la mgongo lakini kwasasa ni wazi kuwa Fernando atashiriki mbio hizo za kuelekea mwishoni mwa msimu.
Rais wa kampuni ya Ferrari, Luca Di Montezemolo ameeleza kufurahishwa na maendeleo ya dereva huyo katika uponaji wake na kwamba wanaendelea kumfuatilia kwa ukaribu na iwapo atakuwa fiti mpaka siku ya Jumapili watamruhusu ashindane.