China: Mafuriko yaua watu ishirini na tisa Hebei
Idadi ya waliofariki kutokana na mafuriko katik mkoa wa Hebei kaskazini mwa China imeongezeka na kufikia angalau 29, vyombo vya habari vya serikali vimeripoti hivi punde Ijumaa usiku, baada ya mvua kubwa kunyesha katika eneo hilo katika wiki za hivi karibuni.
Imechapishwa:
"Tangu Agosti 10, watu 29 wamefariki kutokana na majanga katika mkoa wa Hebei, ambapo 6 hawajulikani waliko. Kufikia sasa idadi ya watu waliokosekana ni 16," shirika la utangazaji la serikali CCTV limeripoti, likinukuu mamlaka ya mkoa wa Hebei.
Takriban watu 33, wakiwemo wafanyakazi wawili wa uokoaji, walifariki mjini Beijing kutokana na dhoruba kali na mafuriko mwishoni mwa mwezi uliopita, mamlaka ilisema wiki hii.
Zaidi ya watu kumi na wawili pia walifariki katika jimbo la Jilin, kaskazini mashariki mwa nchi hiyo, baada ya mvua kubwa kunyesha wiki iliyopita.
Siku ya Ijumaa, Shirika la Habari la New China limeripoti kwamba timu nyingine ya kudhibiti mafuriko imetumwa katika Mkoa jirani wa Liaoning, ambako "hali bado ni mbaya kutokana na mafuriko".
Mitaa katika sehemu za mkoa wa Hebei, pembezoni mwa Beijing, ilikuwa imefunikwa na matope tangu siku ya IJumatano kulingana na shirika la habari la AFP.
Wakazi wanatatizika kuokoa mali zao na kusafisha nyumba zao zilizoharibiwa.
Mamilioni ya watu wamekumbwa na hali mbaya ya hewa na mawimbi ya joto ya muda mrefu kote ulimwenguni katika wiki za hivi karibuni, matukio ambayo wanasayansi wanasema yanachochewa na mabadiliko ya tabia nchi.
Vyombo vya habari vya serikali ya China vimepongeza juhudi za serikali za kupunguza uharibifu wa mafuriko, vikiangazia suala la misaada ya pande zote na maafisa waliojitolea wanaofanya kazi bila kuchoka katika shughuli za uokoaji.