Urusi yatoa wito kwa Washington kukomesha kurusha ndege karibu na mipaka yake
Balozi wa Urusi nchini Marekani Anatoly Antonov alitoa wito kwa Washington kusitisha kile alichokiita safari "za uhasama" karibu na mipaka ya Urusi, baada ya ndege isiyo na rubani ya Marekani iliyonaswa na ndege za kivita za Urusi kuanguka siku moja kabla katika Bahari Nyeusi.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Urusi imeonya kile ilichokiita uhasama wa ndege za Marekani.
"Tunafikiri kwamba Marekani itaepuka uvumi zaidi katika vyombo vya habari na itasitisha safari za ndege karibu na mipaka ya Urusi," Antonov amesema katika taarifa yake kwenye Telegram.
"Tunachukulia hatua zozote za utumiaji wa silaha za Marekani kama uhasama ulio wazi," amesema.
"Urusi haitafuti makabiliano na inasimamia ushirikiano wa kimantiki kwa maslahi ya watu wa nchi zetu," Antonov ameongeza.
Marekani siku ya Jumanne ilishutumu ndege ya Urusi kwa "kunasa na kugonga" ndege isiyo na rubani ya Marekani Reaper juu ya Bahari Nyeusi na kusababisha chombo hicho kuanguka.
Ndege za kivita za Urusi hazikutumia silaha zao
Urusi imekanusha shutuma hizo, huku ikikiri kwamba ndege zake mbili za kivita zilinasa ndege isiyo na rubani ya Marekani ambayo iligunduliwa "katika eneo la rasi ya Crimea" na ilikuwa ikisonga mbele "kuelekea" kwenye mipaka ya Urusi.
Washington imeilaumu Moscow kwa tukio hilo, ikikiita kitendo cha marubani wake kuwa cha kizembe, lakini Urusi imekanusha kufanya ubaya wowote.
Hata hivyo Wizara ya Ulinzi ya Marekani ilisema droni yake ilikuwa kwenye operesheni ya kawaida wakati ilipokatizwa katika njia ya kizembe, isiyo ya mazingira mazuri na isiyokuwa ya kitaalamu.