Ukraine yapongeza Moscow na nchi za Magharibi kwa 'juhudi' za kutuliza mzozo
Ofisi ya rais wa Ukraine imesifu leo Jumanne "juhudi" za Marekani, NATO na Urusi zinazolenga kupunguza mvutano karibu na Ukraine, kama sehemu ya mfululizo wa mazungumzo ya Urusi na nchi za Magharibi wiki hii.
Imechapishwa:
"Tunaweza tu kukaribisha nia na juhudi za Marekani na Urusi, NATO na Urusi kupunguza mivutano na kutatua masuala yote ya pamoja kwenye meza ya mazungumzo," amesema msemaji wa Rais Sergey Nikiforov katika taarifa yake ya video iliyotumwa kwa shirika la habari la AFP.
Siku ya Jumapil Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Antony Blinken aliionya Urusi kuhusu hatari ya "makabiliano" kabla ya kuanza kwa mazungumzo yenye mvutano mkali mjini Geneva kuhusu hali ya Ukraine.
"Kuna njia ya mazungumzo na diplomasia kujaribu kutatua baadhi ya tofauti hizi na kuepuka makabiliano," Antony Blinken amekiambia kituo cha habari cha CNN. "Njia nyingine ni ya makabiliano na matokeo makubwa kwa Urusi ikiwa itaanzisha tena uchokozi wake dhidi ya Ukraine. Tuko katika hatihati ya kuona ni njia gani Rais Putin yuko tayari kuchukua, "alisema Antony Blinken.