Putin: Uchunguzi wa madai ya sumu dhidi ya Navalny ni "hila" ya kushambulia Urusi
Rais wa Urusi Vladimir Putin amesema kwamba uchunguzi uliofanywa na waandishi wa habari, ukiwatuhumu maafisa wa usalama wa serikali kuwa walimpa sumu mpinzani wake Alexei Navalny, ilikuwa "hila" ya kushambulia viongozi wa nchi hiyo.
Imechapishwa:
Kiongozi wa upinzani na mkosoaji mkubwa wa Kremlin Alexei Navalny, siku ya Jumatatu alibaini kwamba ukweli kuhusu sumu aliyopewa umeanzishwa, baada ya kuchapishwa kwa matokeo ya uchunguzi na vyombo kadhaa vya habari ambavyo vimehusisha maafisa wa idara ya usalama nchini Urusi (FSB), ambayo ilikuwa ikimpeleleza Alexei Navalny kwa miaka kadhaa.
FSB, ambayo ilichukuwa nafasi ya KGB wakati wa enzi ya Jamhuri ya Kisovyeti ya Kirusi, haijatoa maelezo kuhusiana na tuhuma hizo.
Kremlin imekuwa ikikanusha madai ya kumuua mmoja wa wapinzani wakuu wa rais Vladimir Putin, ambaye alipoteza fahamu Agosti mwaka huu wakati alikuwa akisafiri kwa ndege akitokea Siberia kwenda Moscow.
Siku mbili baada ya hali yake kuzidi kudhoofika, Alexeï Navalny alisafirishwa nchini Ujerumani, ambako anaishi kufikia sasa baada ya kutibiwa kwa karibu mwezi mmoja katika hospitali ya Charité huko Berlin.