Watu 40 wauawa kufuatia machafuko yanayoendelea nchini Iraq
Watu 40 wameuawa jumanne hii nchini Iraq wakiwamo wapiganaji 13 ambao wameuawa kaskazini mwa nchi hiyo wakati wakitekeleza shambulio la kulipiza kisasi katika vituo vya ukaguzi wa polisi. Taarifa toka nchini humo zinaeleza wapiganaji hao walikasirishwa na mapambano ya awali kati ya waandamanaji na polisi ambayo yalisababisha vifo vya watu 27.
Imechapishwa:
Mapigano hayo yamezuka saa chache baada ya Mwakilishi wa Umoja wa Mataifa UN Martin Kobler kutoa wito kwa pande zote kuwa na uvumilivu ili kurejesha utulivu katika eneo hilo.
Maofisa nchini humo wamearifu kuwa maandamano hayo katika mji wa Hawijah yalikuwa na baadhi ya wahalifu, madai ambayo yamepingwa vikali na waandamanaji wanaodai hawakujumuika na watu hao wanaotafutwa.
Waandamanaji wanadai jeshi limekuwa likitumia nguvu katika kukabiliana nao suala ambalo linahatarisha usalama wa baadhi ya raia wengine wasiokuwa na hatia.
Kwa zaidi ya miezi minne sasa waandamanaji nchini Iraq wameendelea kupaza sauti zao wakimtaka Waziri Mkuu wa nchi hiyo Nouri al-Maliki ajiuzulu.