Idadi ya watu waliouawa katika shambulio jijini Moscow imefikia 115
Nairobi – Idadi ya watu waliopoteza maisha kufuatia shambulio lililotekelezwa na watu wenye silaha kwenye jumba lililokuwa linaandaa tamasha la muziki, nje kidogo ya jiji la Moscow nchini Urusi hapo jana, sasa imeongezeka na kufikia 115.
Imechapishwa:
Maafisa nchini Urusi wanasema, idadi ya vifo huenda ikaongezeka kufuatia shambulio hilo ambalo limewaacha watu wengine zaidi ya 100 na majeraha mabaya.
Tayari watu zaidi ya 10 wamekamatwa, wakiwemo wanne, wanaodaiwa kuhusika moja kwa moja na shambulio hilo ambalo kundi la Islamic State linadai kuhusika.
Licha ya kuwapiga risasi watu waliokuwa kwenye tamasha hilo, watu hao wenye silaha walitumia kemikali kuwasha moto ukumbi huo.
Rais Vladimir Putin ameelani shambulio hilo alilosema ni la kigaidi na kuahidi kuwa waliohusika watachukuliwa hatua kali.
Aidha, Putin ametangaza maombolezo ya kitaifa, huku akiongeza kuwa walioshambulia watu walikuwa wanajaribu kukimbilia nchini Ukraine.
Marekani imesema ilitoa onyo kwa Urusi na kuwapa taarifa za Kiinteljensia mapema mwezi huu kuhusu kuwepo kwa mpango wa kutekeleza mashambulio yanayolenga mikusanyko mikubwa ya watu.
Afisa mmoja wa usalama wa urusi amesema Urusi ilipokea onyo kuhusu shambulio hilo, lakini halikueleza ni wapi walipolenga.
Viongozi mbalimbali duniani, wakiongozwa na rais wa China Xi Jinping, ambaye ni mshirika wa karibu wa rais Putin wametuma salamu za pole kwa watu wa Urusi na kulaani shambulio hilo.