Coronavirus: Idadi ya vifo yapindukia 100,000 nchini Marekani
Idadi ya watu waliopoteza maisha nchini Marekani kutokana na virusi vya Corona, imeongezeka na sasa kufikia zaidi ya watu 100,000 kwa muda wa karibu miezi minne.
Imechapishwa:
Hii inaifanya Marekani kuwa taifa lenye idadi kubwa ya vifo vinavyotokana na virusi hivi ambavyo vimeendelea kuitesa dunia, kwa mujibu wa takwimu zilizotangazwa na Chuo Kikuu cha Johns Hopkins.
Mbali na vifo hivyo, Marekani ina maambukizi zaidi ya Milioni 1 nukta 6 ambayo ni asilimia 30 ya maambukizi yote duniani.
Wiki kadhaa zilizopita rais Donald Trump alisema nchi yake kuwa na visa vingi vya maambukizi ni kitendo cha heshima kwa taifa hilo.
Joe Biden, Makamu wa rais wa zamani ambaye atapambana na rais Trump wakati wa Uchaguzi Mkuu mwezi Novemba, ameendelea kumlaumu kiongozi huyo kwa kushindwa kufanya maamuzi sahihi kukabiliana na janga hili.
Duniani, idadi ya watu waliopoteza maisha imefikia zaidi ya 354,983 huku wengine zaidi ya Milioni 5.6 wakiambukizwa.