Côte d'Ivoire: Matokeo ya mwisho yathibitisha Ouattara kashinda uchaguzi wa urais
Matokeo ya mwisho ya uchaguzi wa urais nchini Cote d'Ivoire yanathibitisha ushindi wa Alassane Ouattara kwa 94.27% ya kura, Mahakama ya Katiba ya Côte d'Ivoire imetangaza leo Jumatatu.
Imechapishwa:
Uchaguzi wa Oktoba 31 ulifanyika katika hali ya wasiwasi, na viongozi wakuu upinzani wa rais anayemaliza muda wake walitoa wito wa kususiwa kwa uchaguzi huo.
Upinzani unabaini kwamba Alassane Ouattara alikiuka Katiba, ambayo inapiga marufuku rais kuwania mihula mitatu mfululizo. Rais anayemaliza muda wake amejibu kwamba katiba mpya iliyopitishwa mwaka 2016 iliondoa marufuku hayo, na kumruhusu kugombea tena.
Waziri Mkuu wa zamani Pascal Affi N'Guessan, mmoja wa viongozi wa upinzani, alikamatwa usiku wa Ijumaa kuamkia Jumamosi baada ya kutangaza uundwaji wa serikali ya mpito, mkewe na mmoja wa wasemaji wake wamebaini.