Coronavirus: Mahakama ya Afrika Kusini yatoa siku 14 kwa serikali kupitia upya masharti yake
Mahakama ya Afrika Kusini imebaini kwamba hatua kadhaa za serikali katika kukabiliana na maambukizi ya Corona ni "kinyume na Katiba ya nchi na ni batili".
Imechapishwa: Imehaririwa:
Jaji amezitaja hatua kuhusu mazishi na wafanyakazi wasio rasmi, kuwa "hazina maana".
Serikali ina siku 14 za kurekebisha hatua hizo, kulingana na mahakama hiyo.
Hapo awali Afrika Kusini ilichukua hatua kadhaa za watu kutotembea, hatua ambazo ni kali zaidi duniani.
Nchi hii ina kesi 35,812 za maambukizi ya virusi vya Corona zilizothibitishwa na vifo 755.
Kesi hiyo iimepelekwa mahakamani na mashirika yasiyo ya kiserikali ya Liberty Fighters na Hola Bona Renaissance Foundation.
Mahakama Kuu ya mji mkuu, Pretoria, imeamua kwamba hatua hizo hazihusiani na kupunguza kwa kasi kwa maambukizi au kupungua kwa kusambaa kwa ugonjwa huo.
"Hatua hizo ... katika idadi kubwa ya kesi hazijahusishwa na malengo ya kupungua kwa kasi kwa maambukizi au kupungua kusambaa kwa ugonjwa", imeandikwa kwenye uamuzi huo.
Jaji Norman Davis amesema kuwa ni makosa kuruhusu watu kusafiri kwenda kwenye mazishi lakini sio kwenda kutafuta pesa kwa kufanya biashara za mitaani, kama wanavyofanya raia wengi wa Afrika Kusini.
Serikali imesema itapitia upya hatua hizo, lakini kwa kusubiri, hatua zilizopo zitaendelea kutumika.