Volodymyr Zelensky ahimiza G7 kumaliza vita kabla ya mwisho wa mwaka
Katika Kasri la Elmau huko Bavaria, Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky Jumatatu (Juni 27) amewataka Wakuu wa nchi na Serikali wa G7 "kufanya kila wawezalo" kumaliza vita vinavyoharibu nchi yake kabla ya mwisho wa mwaka, vilisema vyanzo kutoka kundi la mataifa ya G7 yenye viwanda vikubwa duniani, limeripoti shirika la habari la AFP.
Imechapishwa:
Kiongozi wa Ukraine, ambaye amezungumza kwa njia ya video siku ya Jumatatu katika Kasri ya Elmau, kusini mwa Ujerumani ambapo viongozi wa nchi saba zilizoendelea kiviwanda wanakutana, "alikuwa na ujumbe mzito kwa kusema kwamba watalazimika kufanya kila zawezalo kujaribu kukomesha vita hivi kabla ya mwisho wa mwaka,” limeripoti shirika la habari la AFP, likinukuu vyanzo kutoka G7.
Volodymyr Zelensky "pia alisisitiza juu ya hitaji la kuzidisha vikwazo dhidi ya Urusi", kulingana na vyanzo hivi, akisisitiza umuhimu "wa kutopunguza shinikizo na kuendelea kuchukuwa vikwazo kwa kiasi kikubwa dhidi ya Urusi". Wakati wa hotuba yake, rais wa Ukraine "alirejelea msimu wa baridi kali" huko Ukraine "ambapo ni vigumu kupigana". "Mwishoni mwa mwaka, tutaingia katika hali ambayo tutalazimika kuondoka kwenye ngome zetu", vinaonyesha vyanzo hivi.
Kwa upande wao, viongozi wa G7 wameahidi "kuendelea kutoa msaada wa kifedha, kibinadamu, kijeshi na kidiplomasia" kwa Ukraine "kwa muda mrefu iwezekanavyo", katika taarifa ya pamoja iliyotolewa katika mkutano wao wa kilele huko kusini mwa Ujerumani. Pia wamonyesha "wasiwasi wao mkubwa" baada ya tangazo la Urusi kwamba inaweza kuhamisha makombora yenye uwezo wa nyuklia hadi Belarus.