Mkimbizi wa Syria nchini Ujerumani ajiua
Maafisa nchini Ujerumani wanasema raia wa Syria aliyenyimwa hifadhi nchini humo alijiua na kuwajeruhi watu wengine 12 baada ya kujilipua kwa bomu katika tamasha la muziki mjini Ansbach.
Imechapishwa:
Wizara ya Mambo ya ndani imethibitisha kujilipua kwa mwanaume huyo mwenye umri wa miaka 27, baada ya kukatiliwa pia kuingia katika tamasha hilo mwishoni mwa wiki iliyopita.
Tukio hilo lilisababisha zaidi ya watu 2,000 kuondolewa katika eneo hilo burudani kwa hofu ya kutokea kwa shambulizi la kigaidi.
Hii ni mara ya tatu kwa Ujerumani kushuhudia mashambulizi ndani ya kipindi cha wiki moja.
Haijafahamika ikiwa raia huyo wa Syria alikuwa amepanga kujiua au kuwauwa watu katika tukio hilo.
Ijumaa iliyopita, shambulizi la kigaidi katika jengo la kibiashara mjini Munich lilisababisha vifo vya watu 9 na kuwajeruhi wengine.
Ujerumani imetoa hifadhi kwa maelfu ya wakimbizi kutoka Syria ambao wamekimbia nchi yao kwa sababu ya vita vinavyoendelea katika nchi yao.