Watu kadhaa wajeruhiwa katika shambulio karibu na mji wa Jerusalem
Polisi nchini Israeli wamethibitisha kujeruhiwa kwa watu kadhaa katika shambulio la watu wenye silaha kwenye kituo cha ukaguzi karibu na mji wa Jerusalem.
Imechapishwa:
Kwa mujibu wa taarifa ya maofisa wa afya, watu wanne wanauguza majeraha ya risasi, mtu mmoja kati yao akijeruhiwa vibaya kwenye tukio hilo.
Aidha polisi imethibitisha kuwa watu wote waliojeruhiwa walikuwa walinda usalama.
Shambulio hili katika kituo cha jukaguzi kinachouunganisha Ukingo wa Magharibi na Jerusalem limetokea ikiwa ni siku ya 41 tangu kuanza kwa vita kati ya Hamas na jeshi la Israeli.
Israeli imeapa kuwamaliza wapiganaji wa Hamas waliotekeleza shambulio dhidi yake tarehe saba ya mwezi Oktoba ambapo watu 1,200 waliuawa wengi wao wakiwa ni raia wa kawaida kwa mujibu wa mamlaka ya Israeli.
Hamas pia waliwateka karibia watu 240 baadhi yao wakiwa ni watoto na watu wakongwe kama iliyothibitisha mamlaka nchini humo.
Katika upande mwengine, wizara ya afya katika ukanda wa Gaza inayoongozwa na Hamas, imesema idadi ya watu waliouawa katika mashambulio ya Israeli imefikia 11,500 wakiwemo watoto.