Panetta aruhusu wanajeshi wanawake wa Marekani kushiriki vita mstari wa mbele
Waziri wa ulinzi wa Marekani Leon Panetta ametangaza kuondoa marufuku iliyokuwa imewekwa na wizara yake ambayo inawazuia wanawake kuwa mstari wa mbele kwenye vita.
Imechapishwa:
Waziri Panetta amesema kuwa uamuzi wa kuondoa marufuku hiyo umetokana na umahiri ambao umeoneshwa na wanajeshi wanawake wa nchi hiyo waliothibitisha kuwa wanaweza kushiriki mstari wa mbele kwenye vita.
Msemaji wa wizara hiyo ameongeza kuwa kutokana na wanawake wengi kushiriki kwenye vita vya Afghanistan na kule nchini Iraq, wameonesha uwezo mkubwa wa kushiriki kikamilifu mstari wa mbele katika kuongoza mapambano jambo ambalo hawaoni kwanini wasiwape nafasi hivi sasa.
Rais Barack Obama ambaye kwenye hotuba yake ya mara baada ya kuapishwa alitaka kila mwananchi kupewa nafasi amepongeza uamuzi wa wizara hiyo wa kuamua kuwapa nafasi wanawake ili kudhihirisha uwezo wao kwenye mapambano.
Awali wizara hiyo ilikuwa imeweka marufuku kwa wanawake kushiriki mstari wa mbele kwenye vita badala yake walikuwa wakishiriki kusaidia wanajeshi waliojeruhiwa na kimawasiliano.
Wachambuzi wa masuala ya usalama wanaona kuwa hatua hiyo itachangia kutoa fursa hata kwa mataifa mengine ambayo yamewanyima haki wanawake kushiriki mstari wa mbele kwenye vita jambo ambalo wanadai kwasasa ni lazima nchi zitoe vipaumbele.