Korea Kaskazini yatishia kutekeleza majaribio zaidi ya makombora ya masafa marefu
Serikali ya Korea Kaskazini siku ya alhamisi imetangaza kuwa na mpango wa kutekeleza jaribio lake la tatu la kombora la masafa marefu mpango ambao unailenga nchi ya Marekani.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na wizara ya ulinzi ya nchi hiyo imesema kuwa Korea Kaskazini inapanga kutekeleza jaribio jingine la masafa marefu kama mpango wake wa kuendelea kuboresha teknolojia yake.
Kauli ya nchi hiyo kutaka kujaribu kombora jingine inakuja ikiwa zimepita saa chache toka baraza la usalama la Umoja wa Mataifa UN liidhinishe vikwazo zaidi dhidi ya nchi hiyo kutokana na kuendelea kukaidi maazimio ya Umoja huo kuhusu mpango wake wa Nyuklia.
Wachambuzi wa mambo wanaona kuwa kitisho cha Korea Kaskazini kitaendelea kuweka shinikizo zaidi toka kwa mataifa ya Magharibi ambayo yametaka kuendelea kushukuliwa kwa hatua zaidi dhidi ya taifa hilo.
Hata hivyo wachambuzi hao wanaona kuwa hatua ya Korea Kaskazini kuendelea na vitisho vya kujaribu kombora jingine linailenga nchi ya Marekani ambayo imekuwa kinara katika kuhakikisha taifa hilo linawekewa vikwazo zaidi.