Maandamano jijini Nairobi kulalamikia madai ya ubakaji Hospitali ya taifa
Kumekuwa na maandamano ya wanaharakati wa kutetea haki za binadamu na wawakilishi wa wanawake jijini Nairobi nchini Kenya, kulaani madai ya kubakwa na kunyanyaswa kimapenzi kwa akina mama wanaojifungua katika Hospitali ya taifa ya Kenyatta.
Imechapishwa:
Wanaharakati hao wanataka kujiuzulu kwa Waziri wa afya Cleopa Mailu na Mkurugenzi Mkuu wa Hospitali hiyo Lily Koross kutokana na madai hayo.
Mamia ya waandamanaji hao walipokewa na wafanyikazi wa Hopsitali hiyo na kuanza kuzozana vikali kwa maneno walipojaribu kuingia ndani ya hospitali hiyo.
Maafisa wa usalama wamekuwa wakichunguza madai hayo yaliyoanza kujadiliwa kupitia mitandao ya kijamii wiki iliyopita, lakini ripoti zinasema kuwa, hakuna mwanamke hata mmoja aliyejitokeza kulalamikia madai hayo.
Wafanyikazi wa hospitali hiyo wamepinga madai hayo na kusema kuwa wanaharakati hao wamelipwa.