Ripoti: Kiwango cha demokrasia Afrika Mashariki kimeshuka
Kiwango cha demokrasia kimeshuka kwa kiasi kikubwa barani Afrika hasa miongoni mwa mataifa ya Afrika Mashariki na Kati.
Imechapishwa:
Ripoti iliyotolewa na Shirika lisilokuwa la kiserikali la Fredoom House lenye makao yake jijini Washington DC nchini Marekani, katika ripoti yake ya hali ya demokrasia duniani kwa mwaka 2017, imeyataja mataifa ya Kenya na Tanzania kuwa miongoni ambayo hali ya demokrasia imeshuka.
Uchaguzi Mkuu nchini Kenya mwaka 2017, umechangia pakubwa kwa kushuka kwa viwango vya demokrasia kwa namna zoezi hilo lilivyofanyika.
Masuala yaliyochangia kudorora kwa demokrasia nchini Kenya ni uchaguzi tata wa urais uliompa ushindi rais Uhuru Kenyatta, lakini pia hatua ya wanasiasa kutishia uhuru wa Mahakama na Tume ya Uchaguzi.
Uchaguzi wa marudio ulisusiwa na kiongozi wa NASA Raila Odinga, baada ya kudai kuwa kulikuwa na mpango wa wizi wa kura katika Uchaguzo huo uliofanyika mwezi Oktoba.
Mahakama ya Juu ilifuta ushindi wa Uchaguzi wa kwanza uliofanyika mwezi Agosti, baada ya kubaini kuwa rais Kenyatta hakushinda kwa haki.
Nchini Tanzania, hali hiyo imeshuka tangu kuingia madarakani kwa rais John Magufuli mwaka 2015.
Serikali ya Magufuli imeendelea kushtumiwa kwa kuminya haki za raia kujieleza na kuikosoa serikali, kuwazuia wanasiasa wa upinzani na kupiga marufuku mikutano ya kisiasa.
Ripoti hiyo imeeleza kuwa wananchi wa Tanzania pia wamekuwa wakikamatwa kwa kumkosoa Magufuli kupitia mitandao ya kijamii.
Uganda imeimarika kutoka katika nchi ambayo sio huru kabisa hadi huru kidogo.
Mataifa mengine ya Afrika Mashariki na Kati ambayo kiwango cha demokrasia kipo chini ni Rwanda, Burundi, Somalia na Sudan Kusini kutokana na hali ya kisiasa katika mataifa hayo.
Kwingineko barani Afrika hali ya demokrasia nchini Zimbawe imeshuka, baada ya jeshi kumwondoa madarakani rais wa zamani Robert Mugabe.
Hata hivyo, Gambia ndio iliyoimarika zaidi baada ya kuapata alama 21 baada ya kukubali kuondoka madarakani kwa rais wa zamani Yahya Jammeh na kuingia madarakani kwa rais wa sasa Adama Barrow.