Mgomo wa Wauguzi nchini Kenya wawalazimu wagonjwa kutafuta huduma Tanzania
Wagonjwa kutoka Kaunti ya Taita Taveta na Kwale Pwani ya Kenya wanalazimika kuvuka mpaka na kuingia nchi jirani ya Tanzania kupata huduma za afya kutokana na mgomo wa Wauguzi unaoendelea.
Imechapishwa:
Huduma za afya zimekwama katika Hospitali mbalimbali za serikali Pwani ya Kenya na Kaunti zingine nchini humo kwa sababu wanataka kutekelezwa kwa mkataba wa kuwaongezea mshahara kama ilivyokubaliwa mwezi Machi.
Sekta ya afya nchini Kenya inashughulikiwa na serikali za Kaunti zinazosimamiwa na Magavana.
Wiki iliyopita, Baraza la Magavana nchini Kenya lilitoa wiki moja kwa Wauguzi hao kurudi kazini la sivyo watafutwa kazi.
Chama cha Wauguzi nchini humo kinasema kuwa wafanyikazi wake 25,000 wanaogoma hawatarudi kazini hadi pale matakwa yao yatakaposhughulikiwa.
Wanataka pia kuimarishwa kwa mazingira yao ya utendakazi.
Mgomo huu umekuwa ukiendelea tangu mapema mwezi Juni.