Serikali ya Juba yapuuza wito wa Umoja wa Mataifa
Serikali ya Sudan Kusini imepuuza onyo la Umoja wa Mataifa kutokana na hatua ya rais Salva Kiir kumteua Jenerali Taban Gai Deng kuwa Makamu wa kwanza wa rais kuchukua nafasi ya Riek Machar.
Imechapishwa:
Msemaji wa serikali na Waziri wa Habari Samuel Makuei amesema uteuzi wa Deng lilikuwa ni jukumu la upinzani wala sio la serikali.
Makuei amesisitiza kuwa Jenerali Deng ambaye aliwaakilisha waasi katika mazungumzo ya amani mwaka uliopita, anamwakilisha Machar katika serikali hiyo ya mpito.
Umoja wa Mataifa umemwonya rais Kiir kwa kufanya uteuzi huo ambao umekwenda kinyume na mkataba wa amani na ambao unaweza kuzua vita nchini humo.
Machar ambaye hajulikani aliko, naye amelaani uteuzi huo na kusema kuwa hautambui.
Wachambuzi wa siasa za Sudan Kusini wanaonya kuwa ikiwa mwafaka wa haraka hautapatikana huenda nchi hiyo ikashuhudia mapigano mabaya katika siku zijazo.
Zaidi ya watu 300 walipoteza maisha wengi wao wakiwa wanajeshi wanaomuunga mkono rais Salva Kiir na Riek Machar.