Kenya, Raia wakerwa na ushuru mpya unaowalenga wasafiri
Nairobi – Nchini Kenya, raia wameonekana kupinga agizo la mamlaka ya mapato linalotaka kutoza ushuru bidhaa za kibinafsi au za nyumbani zenye thamani ya $500 (£400) na zaidi kutokana na watalii wanaozuru na raia wanaorejea nchini humo.
Imechapishwa:
Mamlaka ya ukusanyaji ushuru kwenye taifa hilo la Afrika Mashariki (KRA) inasema bidhaa zote ziwe mpya au tayari zimetumika na ni zaidi ya kiasi hicho zitatozwa ushuru.
Raia kwenye taifa hilo wameonekana kukerwa na mpango huo wanaosema haufai na kwamba utawatia hofu watalii.
Baadhi ya wabunge walisema baadhi ya maafisa wa KRA wamekuwa wakichukua fursa ya agizo hilo kuwahangaisha watalii, suala ambalo wamesema linachafua hadhi ya taifa hilo kwenye jukwa la kimataifa.
Waziri wa utalii Alfred Mutua alitaja hatua hiyo ya KRA kuwa mojawapo ya sababu za idadi ya watalii wanaozuru nchini kupungua.
“Wewe nenda Rwanda, hawakusumbui. Je, Rwanda haitoi kodi? Unaenda Afrika Kusini, na hawakusumbui. Huko Dubai, hawakunyanyasi. Kwa hivyo, kwa nini wageni wetu wanakabiliwa na changamoto kama hizi nchini Kenya? Na tunashangaa kwa nini watu hawaji Kenya,” alisema waziri Mutua .
Hii ni hatua ya hivi punde zaidi katika msururu wa ushuru mpya ulioanzishwa na serikali ya rais William Ruto, mpango ambao pia umehusishwa na kuzorota kwa gharama ya maisha nchini humo.
Sera moja ya rais Ruto kabla ya uchaguzi wa mwaka jana ilikuwa ni kupunguza matatizo ya kifedha na ugumu wa uchumi unaowakabili raia wa taifa hilo.