DRC: Mwanajeshi amewaua waombolezaji 13 kijijini Nyakova
NAIROBI – Watu 13 wakiwemo watoto tisa, wameuawa baada ya kupigwa risasi na mwanajeshi aliyewashambulia waombolezaji katika kijiji cha Nyakova, Jumamosi usiku, mkoani Ituri.
Imechapishwa:
Cheza - 00:36
Ripoti zinasema, mwanajeshi huyo ambaye anatafutwa baada ya tukio hilo, alitekeleza kitendo hicho baada ya kugundua kuwa mtoto wake alizikwa bila yeye kuwepo.
Msemaji wa jeshi la DRC, mkoani Ituri, luteni Jules Ngongo, amesema msako umeanzishwa wa kumtafuta mwanajeshi huyo akabiliwe kisheria.
Mwanajeshi kwa mazingira yoyote yale hakuna kati yetu anayohaki ya kuondoa uhai wa ndugu yake. Kulikuwa na tatizo la familia ambalo jeshi lilishindwa kudhibiti kulingana na taarifa tulizonazo.
Ngongo amesema kuwa watoto wawili wa mwanajeshi huyo ni miongoni mwa waliouawa kwa kupigwa risasi, katika kitendo ambacho amekitaja kuwa cha utovu wa nidhamu.
Chifu wa kijiji hicho Oscar Baraka Muguwa, amesema mwanamume huyo alitekeleza shambulio hilo baada ya kurejea kutoka kwa majukumu mengine katika kijiji kingine na kupata wanajamii wakiomboleza kifo cha mwanawe.