Kenya : Akaunti za benki za pasta Ezekiel zazuiliwa na serikali
NAIROBI – Mawakili wa mhubiri anayekabiliwa na utata nchini Kenya, Ezekieli Odero maarufu kama pasta Ezekieli, wamethibitisha kuwa serikali imezuia akaunti za benki 15 zinazomilikiwa na mteja wao, mke wake na za kanisa lake kwa siku 30.
Imechapishwa:
Kwa mujibu wa mahakama, hatua hii imechukuliwa ilikutoa nafasi kwa maofisa wa polisi kukamilisha uchunguzi wao.
Maofisa wa upelelezi wanasema kuwa huenda mhubiri huyo anahusishwa na utakatishaji wa fedha, maofisa hao wakieleza kuwa akaunti hizi zimekuwa zikipokea fedha kwa kiwango kikubwa na huenda zinatokana na shughuli za mhubiri mwengine anayezuiliwa Paul Makenzie.
Ombi la kutaka kuziwa kwa akaunti za mhubiri huyo liliwasilishwa siku ya Jumatatu ya wiki hii na afisa anayechunguza keshi dhidi ya mhubiri huyo, lilipendekeza kuwa akaunti 15 za benki za kiongozi huyo wa dini pamoja na laini saba za kusambaza pesa maarufu kama Mpesa kufungwa.
Polisi wanasema hatua hii imechukuliwa kutokana na madai kwamba huenda pasta Ezekiel anajihusisha na ulaghai kutokana na uhusiano wake wa karibu na Paul Makenzie ambaye miili zaidi ya 100 inayodaiwa kuwa ya wafuasi wake kufukuliwa kwenye shamba lake.
Aidha polisi wanaamini kuwa pesa ambazo zimekuwa zikiingia kwa kiasi kikubwa katika akaunti za Ezekiel Odero pesa hizo zikiaaminika kuwa huenda zimekuwa zikitoka kwa washirika wa Paul Makenzie anayodaiwa kuwa hadaha kuuza mali zao na baadae kumpa pesa zao kwa Kutumia kisingizo cha Imani.
Polisi wanasema kuwa Ezekiel na mshukiwa wa mauaji ya Shakahola, Paul Mackenzie, walishirikiana kupata pesa kutoka kwa biashara haramu ya ulanguzi wa viungo vya binadamu, mbali na kushawishi waumini kuuza mali zao zote kisha kupeleka pesa kanisani.
Miongoni mwa akaunti ambazo mhubiri huyo amezuiwa kutumia, ni nne zilizosajiliwa kwa jina la Kilifi International School iliyojengwa katika kiwanja cha kanisa lake.
Akaunti nyingine 20 zimesajiliwa kwa jina la New Life Prayer Center ambapo baadhi zinashikilia sarafu za pesa za kigeni ikiwemo shilingi ya Tanzania, dola, yuro, na pauni.Akaunti nne za benki ziko kwa jina la Bw Odero, sawa na nyingine saba za M-Pesa.
Polisi wameruhusiwa kuchunguza shughuli zote zilizofanywa kwenye akaunti hizo kwa kipindi cha kuanzia Januari 1, 2017 hadi Aprili 2023 na wasimamizi wa benki zote husika wameagizwa kutoa usaidizi unaotakikana.
Hata hivyo, mawakili wake wakiongozwa na Bw Cliff Ombeta, walikashifu uamuzi huo wakisema uamuzi ulitolewa bila mshtakiwa kuhusishwa.
Maofisa wa upelelezi waliambia mahakama kuwa iwapo hatua hiyo haingechukuliwa huenda mshukiwa angehamisha pesa hizo suala ambalo lingehujumu uchunguzi wao katika keshi hiyo.
Mameneja wa benki ambazo mhubiri huyo ana akaunti wametakiwa kushirikiana na wapelelezi pamoja na kutoa taarifa kuzihusu pamoja na kuzuia utoaji wa pesa kwenye akaunti hizo kumi na tano.
Mawakili wake wameeleza kuwa wataiomba mahakama kuzuia kufungwa kwa kituo cha televisheni kinachomilikiwa na mhubiri huyo pamoja na kutofungwa kwa kanisa lake.