Kundi la pili la wanajeshi wa Kenya lawasili Goma, Kivu Kaskazini
Kundi la pili la wanajeshi wa Kenya, limewasili mjini Goma Mashariki mwa DRC, kuungana na kikosi cha pamoja cha nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki, kusaidiana na jeshi la FARDC kukabiliana na makundi ya waasi ili kuleta utulivu Mashariki mwa nchi hiyo.
Imechapishwa:
Wanajeshi hao wa Kenya, wanaungana na wenzao, waliotangulia kuwasili mjini Goma wiki iliyopita. Kenya imesema inatuma wanajeshi wake 900 Mashariki mwa DRC.
Jumuiya ya Afrika Mashariki katika mkataba wa pamoja, imekubaliana kuwa, wanajeshi wa Kenya watakuwa katika jimbo la Kivu Kaskazini na watashirikiana na wenzao ambao wapo kwenye jeshi la kulinda amani MONUSCO kuwashinda waasi, eneo ambalo linawaasi wa M23.
Wanajeshi wa Uganda ambao tayari wapo Mashariki mwa DRC tangu mwaka uliopita, wanapambana na waasi wa ADF huko Kivu Kaskazini na Ituri.
Wanajeshi wa Burundi tayari wapo katika jimbo la Kivu Kusini na kazi yao ni kuwadhibiti waasi wa RED-Tabara, huku wale wa Sudan Kusini wakipambana na waasi wa Lord Resistance's Army.
Haijawa wazi iwapo Tanzania nayo itatuma wanajeshi wake. Rwanda ambayo ni mwanachama wa Jumuiya hiyo, ilikubaliwa kuwa isitume vikosi vyake baada ya DRC kuishtumu kuwaunga waasi wa M23, madai ambayo inakanusha.