Rais wa zamani wa Afrika Kusini Nelson Mandela afikishwa hospitalini baada ya hali yake kubadilika
Rais wa zamani wa Afrika Kusini Nelson Mandela amelazwa hospitalini kwa mara nyingine tena akiendelea kusumbuliwa na maradhi ya mapafu. Taarifa iliyotolewa katika tovuti ya Ofisi ya Rais nchini humo imebainisha kuwa kiongozi huyo amefikishwa hospitalini mjini Pretoria baada ya hali ya afya yake kudhoofika tena.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Msemaji wa Rais Jacob Zuma, Mac Maharaj amesema Mzee Mandela anashughulikiwa na Madaktari Bingwa ambao wanafanya kila jitihada kuhakikisha kiongozi huyo mzalendo anapata nafuu.
Mapema mwezi April mwaka huu Mandela alikaa hospitalini kwa takribani siku kumi akikabiliwa na maradhi yatokanayo na kuathirika kwa mapafu yake hali inayotajwa kuchangia kuzorotesha afya yake kwa muda mrefu sasa.
Mandela ambaye sasa ana umri wa miaka 94 amekuwa akisumbuliwa na maradhi kwenye miaka ya hivi karibuni ambapo mara kadhaa amefikishwa hospitali kwa matibabu ya maradhi kama hayo ambayo madaktari wanasema yanatokana na umri wake kuwa mkubwa.