Coronavirus: Ufaransa kufunga mipaka yake na nchi jirani kwa siku 30
Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron ametangaza mikakati ya serikali yake kupambana na mamabukizi ya virusi vya Corona nchini humo ambavyo vimesababisha vifo vya watu 148 huku wengine zaidi ya elfu sita wakiambukizwa.
Imechapishwa:
Rais wa Ufaransa ametoa wito kwa raia wa nchi hiyo kupunguza safari zao kuanzia Jumanne mchana kwa siku 15 zijazo.
Watu wanaoishi nchini humo wametakiwa kusalia nyumbani na kulazimika tu kuondoka wakienda sokoni kwenda kufanya kazi au hospitalini.
Aidha, Macron amesema kuwa mpaka wa Ufaransa na mataifa jirani ya Ulaya utafungwa kwa siku 30 zijazo lakini raia wa nchi hiyo wataruhusiwa kurejea nyumbani.
Waziri wa mambo ya ndani nchini humo Christophe Castaner amesema kuwa maafisa wa usalama 100,000 watapiga doria katika maeneo mbalimbali ya nchi hiyo na yeyote atakayepatikana akitembea atalazimiika kueleza sababu ya kufanya hivyo.
Pamoja na masharti haya, rais Macron amesema serikali yake itatoa Euro Bilioni 300 kuwasaidia watu ambao biashara zao zimeathirika na mamabukizi hayo.