Somalia: Rais Sheikh Mohamud amesifia hatua ya kuondolewa kwa vikwazo kuhusu silaha
Rais wa Somalia, Hassan Sheikh Mohamud, hapo jana Jumanne, amekaribisha hatua ya baraza la usalama la Umoja wa Mataifa kupiga kura kuondoa vikwazo vya silaha kwa nchi yake, ikiwa ni zaidi ya miaka 30 baada ya marufuku hiyo kuwekwa kwa mara ya kwanza.
Imechapishwa:
Somalia iliwekewa vikwazo mwaka 1992 ili kudhibiti usambazwaji wa silaha kwa wababe wa kivita waliokuwa wakipigana, ambapo walikuwa wamemuondoa madarakani dikteta Mohamed Siad Barre na kuitumbukiza nchi hiyo ya Pembe ya Afrika katika vita vya wenyewe kwa wenyewe.
Baraza hilo lilipitisha maazimio mawili yaliyoandaliwa na Uingereza - moja ikiwa ni kuondoa vikwazo kamili vya silaha kwa Somalia na lingine kuweka tena vikwazo vya silaha kwa wanamgambo wa Al Shabaab wenye uhusiano na Al Qaeda.
Aidha katika pendekezo hilo, nchi wanachama zinaitaka Somalia kujenga vituo salama vya kuhifadhia silaha ikiwa ni pamoja na ukarabati wa miundombinu iliyoko.
Serikali ya Somalia kwa muda mrefu imekuwa ikiomba vikwazo hivyo kuondolewa ili iweze kuimarisha vikosi vyake kukabiliana na wanamgambo wa Al Shaabab.
Hatua hiyo ya UN imetajwa kuja kwa wakati haswa muda huu ambapo serikali ya Mogadishu imeanzisha vita dhidi ya kundi la Al-Shabaab ambalo kwa muda sasa limekuwa likitekeleza mashambulio nchini humo pamoja na mataifa jirani.