RFI Kiswahili yaadhimisha miaka 13, asante kubwa kwako
Nairobi – RFI Kiswahili inaadhimisha miaka 13 tangu kuzinduliwa kwake na kuanza kurusha matangazo yake mubashara kutoka jijini Dar es salaam nchini Tanzania, kabla ya kuhamia jijini Nairobi nchini Kenya, Februari 2022.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Julai 5, 2010 matangazo ya kwanza ya RFI Kiswahili ikiongozwa na Mkuu wa Idhaa wakati huo David Coffey, yalipasua angaa kwa mara ya kwanza kutoka studio zake za Dar es salaam, kuanzia saa 1 na 30 asubuhi saa za Afrika Mashariki, saa 2 na 30 na baadaye saa 12 hadi saa 1 jioni.
Chini ya kauli mbiu ya, Habari za Dunia zinakuja mpaka mlangoni kwako, wanahabari wa kwanza wa idhaa hii walianza kazi kubwa ya kuleta taarifa za dunia kwa lugha ya Kiswahili, kutokea kitovu chake, eneo la Afrika Mashariki.
Mbali na taarifa za Habari, RFI Kiswahili ambazo idhaa hii imeendelea kukuletea kwa miaka hii yote, kila siku inakuletea Makala yanayokuelimisha kuhusu Afya, Mazingira, Utamaduni, Muziki, namna ya kubaini taarifa za uongo, Michezo na Uchumi.
Victor Abuso, aliyekuwepo miaka 13 iliyopita anakumbuka hali ilivyokuwa siku ya kwanza, “Kuwa miongoni mwa wanahabari wa kwanza wa idhaa hii,” amesema Abuso mmoja wa Wahariri.
Emmanuel Makundi, ambaye pia ni Mhariri, alijiunga miaka miwili baadaye, anawashukuru wapenzi wa RFI kwa uaminifu wao,” Tutaendelea kufanya kinachowezekana, kuwaletea vipindi vitakavyowaelimisha na kuwaburudisha,” amesema Makundi ambaye hukuletea uchambuzi wa kipindi cha Gurudumu la Uchumi.
Victor Robert Wile, aliyekuwa Mhariri Mkuu wa kwanza kati ya mwaka 2010 hadi 2022 wakati RFI Kiswahili ilipohamia jijini Nairobi, katika maadhimishho ya miaka 13, amesema, “ Tunaposherehea miaka 13 ya RFI Kiswahili tuna kila jambo kujivunia kwa kuleta ushindani kwa vyombo vya habari vya Kimataifa vinavyotangaza kwa lugha adhimu ya Kiswahili.
“Ninawatakia kila lakheri wafanyakazi na wasikilizaji wa RFI Kiswahili na zaidi hongera sana The Dream Team,” ameongeza akiwa jijini Dar es salaam.
Ruben Lukumbuka, mmoja pia wa wanahabari wakongwe anawaahidi wapenzi wa RFI Kiswahili, habari moto moto ili kuielewa dunia. “Asanteni sana kwa kuendelea kuwa waaminifu kwetu, “ amesema Lukumbuka.
Benson Wakoli, mwandalizi wa kipindi cha Jua Haki Zako, anawashukuru kwa kuendelea kuwa wasikilizaji wema, “Asanteni kwa kutushika mkono,” amesema.
Uongozi wa RFI Kiswahili, chini ya uongozi wa Mkuu wa Idhaa Robert Minangoy, umeandaa hafla siku ya Ijumaa katika kituo cha utamaduni cha Alliance Francaise, siku ya Ijumaa kuadhimisha miaka 13 ya idhaa hii itakayoambatana na siku ya Kimataifa ya lugha ya Kiswahili.
RFI Kiswahili inaadhimisha miaka 13, kwa shukran nyingi kwa wasikilizaji wake kutoka nchi zote za dunia hasa eneo la Maziwa Makuu kwa kuendelea kuwa waaminifu na kukubali kutembelea na idhaa hii hatua kwa hatua.
Tunawapongeza wafanyakazi wote wa sasa na wa zamani kwa mchango wao usioweza kufutika au kusahaulika katika safari ya kuijenga RFI Kiswahili.