Wahisani wakutana jijini Geneva kujadili hali ya Sudan
NAIROBI – Wahisani wa Kimataifa wanakutana jijini Geneva, kujadili vita nchini Sudan, wakati huu utulivu ukishuhudiwa kwa siku ya pili baada ya makubaliano kati ya wanajeshi na wanamgambo wa RSF ambao kwa mwezi wa tatu sasa wameendelea kupîgana.
Imechapishwa:
Antonio Guteress, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, amesema iwapo vita havitasitishwa na msaada wa haraka kupatikana, Sudan itageuka kuwa eneo la mauaji na uharibifu.
Mkutano huu umeandaliwa na Umoja wa Mataifa, kwa ushirikiano wa nchi za Qatar, Saudi Arabia, Misri na Ujerumani.
Lengo ni kutafuta msaada wa fedha kusaidia hali ya kibinadamu nchini Sudan, baada ya vita kuwaacha mamilioni ya watu bila mahitaji muhimu kama chakula.
Hatua hii imekuja, baada ya mashirika ya misaada ya kibinadamu kusema, yanahitaji Dola Bilioni 2.5 kuwasaidia raia wa Sudan. Mpaka sasa ni asilimia 16 ya msaada huo ndio uliopatikana.
Kwa mujibu wa mashirika ya kutoa misaada, nusu ya raia wa Sudan, karibu Milioni 25 wanahitaji kwa haraka misaada ya kibinamu, wakati huu mzozo huo ukisababisha zaidi ya watu Elfu 2 kupoteza maisha, na wengine Milioni Mbili wamelazimika kuyakimbia makaazi yao, wakiwemo Laki tano ambao wamekimbilia katika mataifa jirani.
Licha ya wito wa amani kutoka kwa mashirika mbalimbali, upande wa jeshi na wanagambo wa RSF wameendelea kupigana na mara chache kuheshimu mikataa ya kusitisha mapigano kwa kipindi kifupi ili misaada ya kibinadamu iwafikie walengwa.