DRC: Raia zaidi ya 400 wafariki kutokana na mafuriko makubwa
Nairobi – Watu 400 wameripotiwa kufa kutokana na mafuriko na maporomoko makubwa ya ardhi katika eneo la mashariki ya Kongo. Mamlaka mashariki mwa DRC zinasema kuwa idadi hiyo inazidi kuongezeka.
Imechapishwa:
Wafanyakazi wa misaada ya kibinadamu nchini DRC, wamepata miili hiyo wengi wakiwa wanawake na watoto katika kijiji cha Bushushu, mashariki mwa nchi hiyo.
Theo Ngwabidje, Gavana katika eneo hilo amethibitisha vifo vya watu hao kwa shirika la Habari la Ujerumani (dpa ) na kusema kuwa huenda vifo zaidi vikaripotiwa.
Vilevile Rais wa nchi hiyo Felix Tshisekedi, ametangaza rasmi kuwa siku ya jumatatu itakua siku maalum ili kuomboleza kama taifa .
Msemaji wa serikali, Patrick Muyaya, ameeleza kuwa baadhi ya mawaziri watakwenda kwenye eneo la tukio kwa ajili ya kupanga shughuli ya utoaji misaada na jinsi ya kusimamia shughuli za kupambana na majanga kama hayo.
Mvua kubwa hushuhudiwa hadi mwisho wa mwezi mei .Hii inakuja wakati huu nchi jirani ya Rwanda pia ikiomboleza vifo vya watu zaidi ya 130, waliofariki kutokana na mafuriko yaliyokumba eneo la magharibi mwa nchi hiyo, ambapo mamia ya nyumba ziliharibiwa.
Maombolezo haya yanafanyika wakati huu Serikali ikiendelea kukadiria hasara iliyotokana na mafuriko hayo, huku shughuli za mazishi pia zikiendelea katika moja ya majanga mabaya zaidi kuwahi kuikumba nchi hiyo.
Aidha wengine mbali na kupoteza ndugu zao, wamesema shughuli za maisha ya kawaida zimekoma rasmi baada ya kupoteza mali nyingi ambazo walikuwa wakizitegemea kukimu familia zao.