Côte d’Ivoire: Mabaki ya wahanga wa mzozo wa baada ya uchaguzi yakabidhiwa familia
Mamlaka ya Côte d’Ivoire imerejesha, Jumatano hii, Machi 8 asubuhi, miili ya wahanga wa ghasia zilizofanywa Machi 2011, wakati wa mzozo wa baada ya uchaguzi wa 2010-2011. Maeneo matatu - Guiglo, Blolequin na Toulepleu - yanahusika katika sherehe hii, iliyoundwa kuashiria kitendo cha upatanisho wa kitaifa.
Imechapishwa:
Kwa jumla, miili 47 na mabaki ya wahanga wa ghasia imekabidhiwa familia zao Jumatano hii, Machi 8. Miili hii ilifukuliwa, baadhi mwaka 2015, kisha kuhamishiwa Abidjan, kwa madhumuni ya uchunguzi wa mapigano mbalimbali yaliyotokea wakati wa mgogoro wa baada ya uchaguzi.
Tangu wakati huo, miili hii ilihifadhiwa kwenye makumbusho (Ivosep) huko Treichville. Ilibidi isafirishwe kwa barabara. Ingawa ripoti za uchunguzi wa maiti hazijawasilishwa kwa familia za wahanga hawa, zoezi hili la kukabidhi miili hii linachukuliwa kama ishara inayoruhusu "wakaazi kuomboleza", amebaini Amadou Coulibaly, msemaji wa serikali na waziri.
Mchakato wa maridhiano
Wakati wa ziara yake huko Duékoué mnamo Novemba 15, 2022, Waziri Mkuu, Patrick Achi, pia alitangaza kwamba familia zitapokea fidia kutoka kwa Serikali. Hadi sasa, wanufaika 4,410 wa watu waliofariki tayari wamepokea faranga za CFA milioni 1 (sawa na euro 1,500) kutoka kwa serikali. "Taarifa hizi zimefanya iwezekane kuanzisha tena majadiliano juu ya mada hii ya mwiko," amesema mmoja wa waangalizii.
Kwa upande wa serikali, inasema marejesho haya yanaanguka ndani ya wigo wa upatanisho. Pia ni njia ya kugeuza ukurasa huu wa giza katika historia ya nchi.