Kenya: Wadukuzi waliingilia mawasiliano ya washirika wa rais William Ruto
NAIROBI – Nchini Kenya ripoti zinasema wadukuzi kutoka Israeli, waliingilia mawasiliano binafsi ya washirika wawili wa rais William Ruto, wakati wa Uchaguzi Mkuu mwaka uliopita.
Imechapishwa:
Cheza - 01:08
Hili limebainika baada ya uchunguzi wa pamoja uliofanywa na wanahabari na ripoti hiyo kuchapishwa katika magazeti ya Haaretz ya Israeli na The Guardian la nchini Uingereza.
Ripoti zinasema, mdukuzi huyo aliingia kwenye mawasiliano ya washirika hao kwa lengo la kukusanya taarifa za kiintelejensia kumhusu Ruto lakini pia kusambaza ujumbe wa kisiasa wa kupotosha dhidi yake.
Waliolengwa katika udukuzi huo ni pamoja na Dennis Itumbi na Davis Chirchir, washauri wa kisiasa wa Ruto na uchunguzi zaidi unasema mawasiliano yao ya barua pepe na Telegram, yaliingiliwa na mdukuzi ambaye amefahamika kwa jina la Tal Hanan.
Hata hivyo, uchunguzi huo haujabaini ni nani aliyewaajiri wadukuzi hao, lakini kiongozi wa wengi katika bunge la Kenya Kimani Ichung’wa amewashtumu viongozi wa upinzani kutoka muungano wa Azimio la Umoja akiwahusisha na wadukuzi hao.
Upande wa upinzani haujazungumzia uchunguzi huo, lakini kiongozi wake Raila Odinga ambaye amekataa kumtambua Ruto kama rais, amekunuliwa akisema muungano huo uliwaajiri wadukuzi kubaini ukweli kuhusu mshindi wa uchaguzi wa urais, anaodai yeye ndiye aliyeshinda.