Wataalam: Kujumuishwa kwa waasi katika jeshi la DRC ni kuzidi kudhofisha jeshi
Watalaam wanaonya kuwajumuisha waasi katika jeshi la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, wakati huu inapopambana na kundi la M23, kwa lengo la kuleta utulivu Mashariki mwa nchi hiyo.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Watalaam wa usalama na siasa wanaonya kuwa, sera hiyo iwapo itafufuliwa tena, sio ya kudumu na sio suluhu ya amani Mashariki mwa nchi hiyo.
Mmoja wa watalaam hao Jacques Djoli amesema, mbinu hii imewahi kutumiwa katika miaka iliyopita, haikusaidia na badala yake ilifanya jeshi la DRC kuwa dhaifu.
Mpango huu ulianza kutumiwa mwaka 2003 baada ya makubaliano yaliyokuja baada ya kumalizikakwa vita vya pili vya Congo, lakini ukasitishwa mwaka 2013 baada ya kuonekana kuwa, hausaidii kuleta utulivu.
Kutekelezwa kwa mpango huo, kunaelezwa pia kulifungua milango ya jeshi la DRC kuvamiwa na hata kusababisha mgawanyiko ndani ya vikosi vya usalama.
Onyo hili linakuja katika kipindi hiki ambacho rais Felix Tshisekedi akiwaambia vijana kujitolea na kuungana na jeshi ili kuwakabili waasi wa M 23.