Rais wa Afrika Kusini akutana na mwenzake wa Ukraine
Rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa, ambaye anakosolewa kwa kutoegemea upande wowote tangu kuanza kwa vita nchini Ukraine, amesema Alhamisi kuwa alizungumza kwa simu na mwenzake wa Kyiv, Volodymyr Zelensky.
Imechapishwa:
Bw Ramaphosa alisema kwenye Twitter kwamba wakuu hao wawili wa nchi "walijadili gharama mbaya ya kibinadamu na athari za kimataifa" za mzozo huo, kufuatia uvamizi wa Urusi ulioanzishwa karibu miezi miwili iliyopita.
"Tunakubaliana juu ya haja ya kumaliza kwa mazungumzo mzozo ambao umeathiri ugavi wa kimataifa na nafasi ya Ukraine kama msafirishaji mkuu wa chakula katika bara letu," amesema.
Afrika Kusini, nchi yenye nguvu ya kidiplomasia katika bara hilo, imedumisha msimamo wa kutofungamana na upande wowote licha ya kulaani mzozo huo kimataifa, ikitetea mazungumzo. Nchi hiyo ilikuwa miongoni mwa nchi nyingine ishirini katika bara hilo kutoshiriki wakati wa kura ya Umoja wa Mataifa kuhusu maazimio mawili kuhusu mzozo huo.
Bw Ramaphosa amesema Bw Zelensky "anapanga uhusiano wa karibu na Afrika katika siku zijazo". Rais wa Ukraine pia ameomba kuzungumza na wanachama wa Umoja wa Afrika, kwa mujibu wa mkuu wa shirika hilo, Rais wa Senegal Macky Sall.