Jeshi la FARDC ladhibiti maeneo yaliyokuwa chini ya udhibiti wa waasi Kivu Kusini
Jeshi la Jamhuri ya kidemokrasia ya Congo limesema limefanikiwa kuyadhibiti upya maeneo ya Chakira na Nyamara, katika nyanda za juu na za kati kwenye wilaya ya Fizi, katika jimbo la Kivu Kusini, tangu Jumamosi iliyopita baada ya kuushambulia muungano wa wanamgambo wa Gumino-Twigwaneho na washirika wao ambao walikuwa wamedhibiti vijiji hivi kwa karibu wiki moja.
Imechapishwa:
Hali hii imezua swali la kuwepo au kutokuwepo kwa jeshi la Burundi katika ardhi ya DRC.
Kwa mujibu wa taarifa ya jeshi nchini DRC, muungano wa wanamgambo wa Gumino-Twigwaneho ni uasi mpya ambao umepata uungwaji mkono wa watu wenye silaha kutoka nchi jirani.
Vyanzo vilivyo karibu na muungano huu vimekuwa vikikanusha haya, na sasa vinalishutumu jeshi la serikali kwa kuegemea baadhi ya makundi ya yenye silaha nchini humo.
Baadhi ya maafisa wakuu wa serikali ya jimbo huko Kivu Kusini wamethibitisha kuingia kwa watu wenye silaha kutoka Burundi katika wiki za hivi karibuni, bila ya kutoa maelezo zaidi kuhusu utambulisho wao, wala nini lengo lao kuvuka mpaka na kuingia nchini humo.
Vyanzo vingine huru vya ndani vinadai uvamizi wa jeshi la Burundi, na kwamba idadi kamili ya wanajeshi walioko DRC bado haijajulikana, kukiwa na uvumi kwamba wanajeshi wa Burundi wasioupungua hamsini walionekana wakivuka mpaka wa DRC wiki mbili zilizopita na kwamba Disemba 20 watu kumi na wawili waliokuwa wamebeba silaha walivuka mpaka wa Luvungi kutoka Burundi.
Chanzo hicho kimesema wapiganaji wa kundi la waasi wa Burundi, Red Tabara, waliopo katika eneo hilo, walirushiana risasi na vikosi hivyo vya Burundi kwenye eneo hilo la mpaka.
Imbonerakure, vijana wa chama tawala nchini Burundi, pia wanashukiwa kushirikiana na Mai-Mai katika eneo hili, taarifa ambayo hata hivyo ni vigumu kuthibitisha. Vyanzo huru vimesema
Serikali ya DRC bado haijatoa Tamko lolote kuhusu suala hili.