Sudan yawakamata mamluki 160 waliokuwa wakijaribu kuingia Libya
Jeshi la Sudan limesema, limewakamata raia 160 katika mpaka wake na Libya waliokuwa wakielekea nchini Libya kufanya kazi kama Mamuluki.
Imechapishwa:
Kupitia taarifa ya jenerali Jaddo Hamdan, amesema raia wa Sudan hawataruhusiwa kuvuka mpaka na kwenda kupigana nchini Libya na kuwa wako makini kuzuia, ulanguzi wa binadamu nchini humo.
Mwishoni mwa mwezi uliopita serikali ya Sudan ilitangaza kwamba inawashikilia mamluki 122 waliokamatwa katika Jimbo la Darfur wakijaribu kwenda nchini Libya kushiriki vita vinavyoendelea nchini humo.
Kulingana na ripoti kadhaa za Umoja wa Mataifa, mamia au hata maelfu ya raia wa Sudan wanashiriki vita mara kwa mara nchini Libya.
Sudan mara kadhaa ilikuwa ikinyooshewa kidole kuhusika na machafuko nchini Libya. Serikali ya umoja wa kitaifa ya Tripoli ilikuwa inashutumu vyama vya Sudan kwa kutuma wapiganaji kusaidia kambi ya mpinzani wake, Marshal Khalifa Haftar, madai ambayo serikali ya Sudan wameendelea kukanusha.
Katika ripoti yake ya mwezi Desemba 2019, Umoja wa Mataifa ulithibitisha uwepo wa wapiganaji wa Sudan wakisaidia kambi ya Marshal Khalifa Haftar lakini pia na kambi ya serikali ya Tripoli.