Alassane Ouattara ashinikizwa kuwania katika uchaguzi ujao, baada ya kifo cha Waziri Mkuu
Viongozi wa chama tawala Cote d'Ivoire wamekubaliana kumshinikiza Rais Alassane Ouattara kuwania muhula wa tatu wa urais katika uchaguzi wa mwezi Oktoba baada ya kifo cha waziri mkuu Amadou Coulibaly.
Imechapishwa:
Ouattara alitangaza mnamo mwezi Machi kuwa hatowania tena urais baada ya miaka 10 ofisini na tayari alikuwa amemteua Coulibaly kuwa mgombea wa chama hicho katika uchaguzi mkuu.
Muda wa mwisho wa kuwasilisha jina la mgombea wa urais ni Julai 31.
Waziri Mkuu wa Cote d’Ivoire, Amadou Gon Coulibaly, alifariki dunia ghafla usiku wa kuamkia leo Alhamisi akiwa na umri wa miaka 61.
Kiongozi huyo mwenye umri wa miaka 61 alikuwa amechaguliwa kuwa mgombea wa chama tawala katika uchaguzi wa mwezi Oktoba, baada ya Alassane Ouattara kusema kuwa hatowania muhula wa tatu.
Rais wa Cote d’Ivoire Alassane Ouattara jana usiku alitangaza kwamba nchi yake imeingia kwenye msiba wa kuondokewa ghafla na Coulibaly ambaye alimteua kuwa mrithi wake katika uchaguzi unaopangwa kufanyika nchini humo mwezi Oktoba mwaka huu.
Waziri Mkuu Amadou Gon Coulibaly alishiriki kwenye kikao cha kila wiki cha Baraza la Mawaziri cha serikali ya Cote d’Ivoire, ghafla hali yake ikawa mbaya na amefariki dunia akipewa matibabu hospitalini.
Bwana Coulibali alifanyiwa upandikizaji wa moyo 2012 na alikuwa ameelekea Ufaransa tarehe 2 Mei ili kuwekewa bomba katika mshipa wake wa damu.
“Nimerudi kuchukua mahala pangu kando ya rais , ili kuendelea na jukumu la kujenga taifa letu”, Amadou Gon Coulibaly alisema aliporudi Alhamisi iliopita.