Nigeria: zaidi ya watu 45 wauawa katika jimbo la Borno
Zaidi ya watu arobaini na tano wameuawa na wengine kadhaa kujeruhiwa baada ya wanawake wawili kujitoa muhanga kwenye soko moja kaskazini mwa nchi ya Nigeria kwenye jimbo la Borno, huu ukiwa ni mfululizo wa mashambulizi ya kundi la Boko Haram.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Shambulio hili lililowalenga wananchi waliokuwa sokoni, ni shambulio la pili kutekelezwa na kundi la Boko Haram katika soko hilo hilo ambapo July mosi mwaka huu watu kumi na tano waliuawa baada ya mtu mmoja kujitoa muhanga.
Shambulio la siku ya Jumanne limetekelezwa wakati huu ambapo wanamgambo wa Boko Haram wameripotiwa kuteka mji mwingine kaskazini mwa nchi hiyo, ikiwa ni muendelezo wa harakati zao za kutaka kurejesha miji iliyochukuliwa na serikali.
Mashambulizi haya yanatekelezwa wakati huu ambapo vyama vya upinzani nchini humo vinakosoa namna ambavyo jeshi na serikali vinashindwa kuwakabili wapiganaji wa Boko Haram ambao wamezidisha mashambulizi na kuendelea kufanya hali ya usalama kaskazini mwa nchi hiyo kuwa tete licha ya hali ya hatari iliyotangazwa.