Serikali ya Burundi yanyooshewa kidole cha lawama
Shirika la kimataifa la kutetea Haki za Binadamu la Human Rights Watch limeelezea wasiwasi wake kuhusu mwanaharakati wa kutetea haki za binadamu nchini Burundi Pierre-Claver Mbonimpa aliyewekwa kizuizini hivi majuzi.
Imechapishwa:
Mbonimpa ambaye ni mwenyekiti wa Chama cha ulinzi wa wafungwa na haki za binadamu cha Aprodh anashtakiwa kueneza uvumi wa uongo dhidi ya serikali, kuhatarisha usalama wa taifa ndani na nje ya nchi.
Hivi karibuni Mbonimpa amesikika kwenye redio binafsi ya RPA ya Burundi akidai kwamba vijana kutoka Burundi wanapokea mafunzo ya kijeshi mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo Kinshasa.
Burundi: Leading Rights Activist Arrested http://t.co/aYWLr91L5o
— Human Rights Watch (@hrw) May 17, 2014
Mkurugenzi wa Shirika la Human Rights Watch nchini Burundi na Rwanda, Carina Tertsakian, amesema serikali ya Burundi, hasa viongozi wa taifa hilo hawataki kukosolewa.
“Serikali ya Burundi haikubali kamwe kukosolewa, hasa ikiwa kwa namna ya wazi kama anavyofanya Mbonimpa, na yeye mwenyewe huwa anazungumzia vitisho dhidi yake, na hii ni ishara mbaya sana kwa wanaharakati wa haki za binadamu kiujumla kwa sababu inatoa ishara dhahiri kuwa serikali haivumilii kukosolewa. Hofu yetu ni kwamba hali inaweza kuwa ngumu zaidi, hayo ni wakati uhuru wa kujieleza na wa kushirikiana vinaminywa sana nchini Burundi”, amesema Tertsakian.
Pierre-Claver Mbonompa amezuiliwa jela, baada ya kusikilizwa mahakamani hapo ijumaa iliyopita kuhusu taarifa zinazohusiana na vijana wanaosadikiwa kuwa ni wafuasi wa chama tawala Cndd-fdd “Imbonerakure” kupewa mafunzo ya kijeshi katika nchi jirani ya Congo.
Hivi karibuni taasisi za Umoja wa Mataifa zlitoa onyo kali dhidi ya serikali ya Burundi na kuituhumu kwamba imekua ikiwapa silaha vijana wa chama tawala Cndd-fdd “imbonerakure”, na kutishia kuwachukulia hatua za kisheria, ikihitajika kuwafikisha mbele ya vyombo vya sheria vya kimataifa wale wote watakao husika na vurugu au ukiukwaji wa haki za binadamu nchini humo.