Mahakama ya Uingereza yawaruhusu wazee waliopigania uhuru nchini Kenya kuishtaki serikali
Wazee watatu raia wa Kenya wanaowakilisha wazee wengine waliopigania uhuru nchini humo chini ya mwavuli wa Mau Mau miaka ya hamsini na sitini wameruhusiwa na Mahakama ya Uingereza kuishtaki serikali hiyo kwa kukiuka haki zao za binadamu wakati wa kipindi cha ukoloni.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Uamuzi huo umetolewa baada ya wazee hao wa Mau Mau Jane Muthoni Mara, Paulo Muoka Nzili na Wambugu Wa Nyingi kuwasilisha ombi lao kutaka kesi hiyo isikilizwe na kuruhusiwa kuishtaki serikali ya Uingereza.
Wazee hao wanaowakilisha mamia ya wazee wengine wanasema wanataka kulipwa fidia kwa kuteswa, kupigwa, kuuliwa na wanawake kubakwa na wakoloni hao kutoka Uingereza.
Jaji Mkuu wa Mahakama iliyotoa uamuzi wa kuendelea kwa kesi hiyo Richard McCombe, amesema wakenya hao wana haki ya kuendelea kuishtaki serikali ya Uingereza.
Wazee hao ambao pia wanataka Uingereza kuwaomba msamaha, wanasema wana ushahidi wa kutosha wa kushinda kesi hiyo.
Wakenya hao pia wamepata ungwaji mkono kutoka kwa Aksofu Mkuu mstaafu wa Afrika Kusini Desmon Tutu akiitaka Uingereza kuajibikia makosa yake wakati wa kipindi cha Ukoloni barani Afrika.