Jeshi la Serikali Congo DR latamba kuua waasi 25 wa Ntaganda
Serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo imesema kuwa imefanikiwa kuwauwa waasi wanaomuunga mkono kiongozi wa waasi jenerali Bosco Ntaganda wapatao 25 katika eneo la mashariki mwa nchi hiyo.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Waasi hao wanaodaiwa kumuunga mkono Ntaganda na muasi mwingi kanali Sultani Makenga waliuawa walipokuwa katika harakati za kuutia katika himaya yao mji wa Bunagana katika jimbo la Kivu Kaskazini.
Msemaji wa serikali Lambert Mende amesemam kuwa waasi hao waliuawa lakini upande wa serikali hakukua na kifo ingawaje huenda kukawa na majeruhi kutokana na makabiliano hayo.
Nchi hiyo ya Afrika Mashariki na Kati imebaki kuwa si imara kiusalama kwa karibu muongo mmoja hata baada ya kumalizika kwa vita vya wenyewe katika nchi jirani za Rwanda na Burundi.
Nchi hiyo pamoja na nchi jirani inakabiliwa na hali ya kuzuka kwa mapigano mapya katika majuma ya hivi karibuni baada ya mamia ya wanajeshi kuasi nan kutoka katika jeshi la serikali kwa madai kuwa hawalipwi vizuri huku wakikabiliwa na ugumu wa maisha.
Baada ya kuasi jeshi, wanajeshi hao wanapambana huku wakimuunga mkono bwana Bosco Ntaganda ambaye anasakwa na mahakama ya uhalifu wa kivita, ICC kwa makosa mbalimbali ikiwemo kuingiza watoto katika jeshi.
Ntaganda awali alipigana na majeshi ya Serikali ya Kongo DR akiwa sehemu ya kikundi cha waasi cha CNDP kilichokua kinaungwa mkono na Rwanda kabla ya kusaini makubaliano.