Waasi wa Mali wajitangazia uhuru baada ya kujitenga
Watu wenye silaha nchini Mali wamefanya shambulizi Kaskazini Mashariki mwa nchi hiyo na kufanikiwa kuwateka Wanadiplomasia saba wakati huu Kundi la Waasi la Tuareg likitangaza rasmi Uhuru wa Kaskzini mwa nchi hiyo.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Wanadiplomasia hao wa Algeria akiwemo Balozi Mdogo na wafanyakazi wengine sita walitekwa na watu wenye silaha wakati huu ambapo Utawala wa Kijeshi chini ya Captain Amdou Haya Sanogo wakiwataka wananchi kuukata Utawala wa Tuareg.
Taarifa ya Tuareg inaonesha eneo la Azawad limejitenga rasmi kuondoka Utawala wa Bamako kipindi hiki ambacho Ufaransa kupitia Waziri wake wa Mambo ya Nje Alain Juppe akitaka njia ya mazungumzo itumike kumaliza utata huo.
Kikundi hicho cha waasi ni miongoni mwa vikundi vya waasi ambavyo vimepata nguvu baada ya kuangushwa kwa utawala wa Mali kwa nguvu za kijeshi baada ya serikali hiyo kushindwa kutimiza majukumu yake ikiwa ni pamoja na kushindwa kulisambaratisha kundi la Tuareg.
Waasi hao wametoa ujumbe wa kulitangaza eneo hilo kuwa ni taifa huru na wamesema wataheshimu mipaka ya maeneo ya majimbo mengine.
Ufaransa ambayo ni mtawala wa zamani wa Mali imesema kuwa haitatambua uhuru wa Azawad mpaka uhuru huo utakapotambuliwa na mataifa ya Afrika.