Umoja wa Mataifa kuanzisha Operesheni ya kusaidia waathiriwa wa machafuko ya kikabila Sudani Kusini
Umoja wa Mataifa hii leo umesema kuwa inaanzisha operesheni maalum ya maswala ya misaada ya kibinadaam ili kuwasaidia takriban watu elfu hamsini walioathiriwa na mapigano ya wenyewe kwa wenyewe katika jimbo la Jonglei, Sudani kusini.
Imechapishwa:
Msemaji wa ofisi ya uratibu wa misaada ya kibinaadam Elizabeth Byrs amesema Mpango huo unalenga kusaidia maelfu ya watu kurejea nyumbani baada ya mapigano kati ya watu wa kabila la Lou Nuer na Murle.
Ndani ya saa 72, wataalam kutoka umoja wa mataifa wametathmini hali ilivyo huko Pibor, Likuangole, Boma ba Waglak.
Nao maafisa nchini Sudani wamesema kuwa zaidi ya watu 3000 waliuawa juma lililopita.
Umoja wa Mataifa na maafisa wa Jeshi la Sudan bado hawajathibitisha idadi kamili ya watu waliouawa hasa kutoka maeneo yanayoelezwa kuwa magumu kufikiwa.
Ikiwa idadi hiyo ya zaidi ya watu 3000 itathibitishwa, itakuwa mapigano makali zaidi kutokea yaliyosababishwa na mapigano ya kikabila kuwahi kutokea Sudani kusini.